Header Ads

VITENDO NDIYO CHANZO CHA MAFANIKIO

Kila mtu amekuwa akitaka kufanikiwa, zunguka leo mitaani kila mtu anaimba wimbo mafanikio, ama kwa hakika kama wimbo huu mafanikio ungekuwa unasikiliza waimbaji hawa wenye sauti nzuri, wenye kujua kuyapangilia maneno yao wakati wanauimba wimbo huu mafanikio basi huyu bwana mafanikio angekuwa ameshawapatia hayo mafanikio. Lakini habari mbaya kwa waimbaji hawa ni kuwa wanamwimbia mafanikio ambae kila siku wanaishi nae, wanatembea nae na kula nae yaani kwa kifupi wapo nae kila siku ila waimbaji hawa hawalitambui hilo.

Kila mtu amekuwa akitaka mafanikio lakini wanaofanikiwa ni wachache, ulishawahi kujiuliza kwa nini pamoja na watu wengi sana kuyataka mafanikio hawayapati ni kwa sababu wanakosa kitu kimoja kikubwa ambacho ndio nguzo kubwa ya mafanikio na msingi mkubwa wa mafanikio na kitu hicho sio kingine bali ni vitendo. Mafanikio huja kutokana na vitendo yaani vitendo au matendo ndipo mafanikio hupatikana. Ndio maana hata katika biblia imeandikwa imani bila matendo imekufa, wakiwa na maana kuwa huwezi kusema una imani bila kutenda imani hiyo.

Leo watu tumekuwa tukitaka mafanikio lakini hatutaki kutenda vile mafanikio  yanataka, leo hii mtu anakuambia nataka kuwa daktari lakini mambo anayofanya hayaendani kabisa na huo udaktari anaousema. Kutokana na kuwa vitendo huleta mafanikio ndio maana watu husema kuwa ni kufanya yaani huwezi kuwa mtu fulani kama hujafanya kile kitu. Katika hili pia biblia imesema “atafutae atapata na abishae atafunguliwa”. Hivyo huwezi kuwa mtu fulani kama hujatenda lile jambo.

Kama unataka kuwa mkulima ni lazima uanze kulima ndipo utakuwa mkulima, huwezi kuwa mfanyabiashara kama hujaanza kufanya hiyo biashara, huwezi kuwa mwandishi kama hujaanza kuandika. hivyo kuwa ni kufanya na kufanya ndio mafanikio. Watu wengi sana tumekuwa hatupati maendeleo kwa sababu tu matendo yetu yamekuwa hayaendani na mafanikio hata kidogo.

Leo hii utamkuta kijana anapiga kelele kuhusu mafanikio lakini hataki kufanya kazi kwa bidii anafanya kazi ilimradi tu anafanya kazi yaani yupo yupo tu hana mpangilio wowote katika kazi yake. Leo hii kutokana na sera ya serikali ya awamu ya tano hapa kwetu Tanzania ukipita huko mtaani wimbo unaoimbwa ni “hapa kazi tu”, lakini jambo ambalo linakuja kushangaza na pengine kuacha viulizo vingi sana maishani ni pale unapokuja kugundua kuwa idadi kubwa ya wale wanaosema hapa kazi tu ndio wasio na kazi wapo wapo tu. Yaani kinachotokea ni kuwa wapo tayari kutamka neno kazi lakini hawapo tayari kufanya kazi hizo.

Swala la kukosekana kwa vitendo linajidhihirisha hata katika elimu ambapo watoto wetu, wadogo zetu na wazazi pia tunakosa vitendo katika elimu. Utakuta mwanafunzi anataka afaulu, tena kwa alama za juu lakini mwanafunzi huyu huyu hafanyi juhudi zozote katika masomo yake husika badala yake anaenda shuleni kwa kuwa tu anapaswa kwenda. Wazazi nao wanataka watoto wao  wafanye vizuri katika elimu lakini wanachofanya ni kulipa ada tu, yaani wao wakishalipa ada basi wanahisi kuwa wamemaliza mchango wao katika elimu jambo ambalo sio, mwanao anahitaji toka kwako vitu vingi na sio ada tu.

Leo hii lazima utambue kuwa vitendo ndio msingi wa mafanikio kama ilivyo katika kukata njaa au kiu ya maji. Huwezi kushiba ikiwa hujala, kiu yako ya maji haiwezi kuisha ikiwa hutokunywa maji. Hivyo tambua kuanzia leo hii usiishie tu kuongea bali toka ukatende na hapo ndipo mafanikio utayaona, kumbuka kuwa ni kufanya.
Nikutakie kila kheri katika kuanza vitendo leo hii.

No comments

Contact us:Email:godfreymtega@gmail.com/WhatsApp-+255758297744/+255716824009 . Powered by Blogger.