Header Ads

Hii Ndio Sababu Ya Wengi Kukosa Ujuzi Katika Uongozi Iwe Kwao Binafsi Au Kwa Wengine.

Uongozi ni sifa ambayo kila mtu angependa kuwa nayo katika maisha yake, lakini ukweli ni kwamba  watu wengi wameamua kuwa wafuasi badala ya kuwa viongozi. Mpaka hapo unaweza ukawa unajiuliza, inawezekana vipi mtu akaamua kuwa mfuasi? Tambua kwamba chochote kile unachokifanya au kutokufanya katika maisha huwa kinatokana na maamuzi yako. Yaani hata kule kwenye kutokufanya jambo pia ni uamuzi. Kwa maana hiyo ni kwamba kufanya na kutokufanya ni uamuzi. Ndio hivyo hivyo pia katika kuamua kuwa mfuasi au kiongozi.

Na wengi kwa miaka kadhaa sasa wamekuwa na maswali mbalimbali kuhusiana na uongozi. Maswali kama vile ; nini ninachohitaji kuwa nacho ili niweze kuwa kiongozi? uongozi una sifa zipi na ni yapi majukumu ya kiongozi? Mimi kama kiongozi nitaweza vipi kuwaongoza  wale waliopo chini yangu? Hayo ni baadhi tu ya maswali machache ambayo wengi wamekuwa wakijiuliza.

Ila ningependa kukwambia tu kwamba kabla haujafikiria au kuwa na wazo la kutaka kuwa kiongozi ni muhimu kwanza ukajifunza kujiongoza wewe binafsi. Kuwa na nidhamu binafsi ni jambo la muhimu sana katika uongozi, Kwani Kamwe hautoweza kuja kufanikiwa katika kuwaongoza wengine katika jambo lolote ikiwa wewe mwenyewe unashindwa kujiongoza. Na kama tujuavyo kwamba; maisha yetu kwa kiasi kikubwa yamekuwa yakiongozwa zaidi kutokana na  ushawishi tunaoupata kutoka kwa jamii zetu na mazingira yetu kwa ujumla. Kwa hiyo, kabla haujafikiria kuwa kiongozi ni muhimu ukafanikiwa kwanza kujiongoza mwenyewe halafu uwe na ushawishi mkubwa kwa wale unaowaongoza , sababu watu hao watakuwa wanafuatilia sana kile utakachokuwa unakifanya ama kukitenda. Na Ikiwa utendaji wako utakuwa mzuri, basi hata utendaji kazi wa wale unaowaongoza utakuwa mzuri pia. Na ikiwa utendaji wako utakuwa mbaya basi tegemea kukutana na hali hiyo hiyo pia kutoka kwa wale waliopo chini yako. Unatakiwa uongoze kwa mfano, kwani hakuna aliye tayari kuongozwa kufanya jambo ambalo kiongozi wake halifanyi. Na sababu kubwa hapo ni kama nilivyokuambia awali kwamba maisha yetu kwa kiasi kikubwa yanaongozwa zaidi na ushawishi tunaoupata kutoka kwa jamii zetu pamoja na mazingira yanayotuzunguka. Iwe kwenye maisha binafsi, kikazi, mahusiano, ndoa, biashara n.k inakupasa ujiongoze mwenyewe kwanza kabla haujafikiria kumwongoza yeyote yule ili uweze kupata ufanisi au matokeo yaliyo bora kutoka kwa yule unayemwongoza.

Unahitaji kuwa na ujuzi kuhusiana na masuala ya uongozi ili kuweza kuwa kiongozi bora na sio bora kiongozi. Kwani wengi wanaojiingiza katika masuala ya uongozi mara nyingi huwa wanakosa ujuzi katika kujiongoza wao binafsi au kikundi fulani na matokeo yake kusababisha kuanguka kwa wao binafsi, kikundi kinachowaongoza, mashirika, taasisi na kufikia hatua ya kushindwa kufikia lengo tarajiwa. Ebu tuangalie sababu inayowafanya wengi wasiwe na ujuzi katika uongozi.

Kwa nini baadhi ya watu wana ujuzi katika uongozi huku wengine wakiwa hawana?
Hilo ni swali ambalo limekuwa likigonga vichwa vya watu wengi kwa muda mrefu sasa na ikiwezekana wewe ukiwa ni mmojawapo. Kwani kuna uwezekano ukawa  umekwishawahi kujiuliza swali la aina hiyo hapo kabla. Na jibu la swali hilo ni kwamba; uongozi ni ujuzi ambao hatuzaliwi nao. Huu ni ujuzi ambao unaweza ukauendeleza na hata kufuzu. Japokuwa kuna uwezekano wa uwepo wa watu wenye vipaji sana linapokuja suala la kuwa kiongozi, lakini jambo la muhimu unalopaswa kulitambua na kulizingatia ni kwamba kila mtu anaweza kuwa kiongozi. Ni maamuzi yako tu ya kuamua kuinuka  ili kupata uzoefu zaidi pamoja na hekima katika uongozi. Jifunze kadri uwezavyo kuhusiana na uongozi na tumia kile utakachojifunza kisha kuwa utahayari wa kuendeleza kile unachojifunza, na matokeo ya wewe kufanya hivyo ni kuja kupata uzoefu pamoja na hekima katika suala zima la uongozi.
Pia ni lazima ujifunze na utambue wewe ni aina gani ya kiongozi.  Unaweza kufahamu wewe ni kiongozi wa aina gani kwa kujitazama wewe binafsi, kwa kuangalia kile unachokifanya au kinachokupa hamasa  ili uweze kujitengenezea nembo yako (brand) .Kwani kuwa na nembo katika zama hizi ni jambo la muhimu sana.  Na ninapozungumzia nembo, nakuwa nazungumzia utambulisho wako. Yaani ujulikane kama kiongozi wa aina gani? Kwa mfano; unaweza ukajulikana kama kiongozi wa masuala yahusuyo  siasa, elimu, maisha, dini n.k.

Watu wengi katika zama hizi wamekuwa sio viongozi na badala yake wamegeuka kuwa kundi la wafuasi, na wameacha kabisa hata kushika hatamu juu ya maisha yao. Yaani wamekubali kabisa kuamriwa jinsi gani wanapaswa waishi maisha yao, na wala  sio watakavyo au wapendavyo wao. Na wengi wamekwenda mbali zaidi kwa kukubali kila jambo linalowatokea katika maisha yao kuwa ni sawa ajari. Mafanikio katika maisha sio ajari bali ni matokeo ya kile unachokifanya siku zote za maisha yako iwe kwa kujua ama kutokujua. Wewe ndiye dereva mkuu wa maisha yako. Kwa hiyo yaongoze maisha yako kuelekea kule unapotaka yawe, na uamuzi ni wako na si wa mwingine kubali au kataa. Hilo ni kosa ambalo wengi wamekuwa wakilifanya kwa miaka kadhaa sasa kwa kuruhusu wengine wayatawale maisha yao huku wakishindwa kutambua jinsi gani linawagharimu maisha yao .Hilo ni kosa ambalo hupaswi kulifanya rafiki.

Ikiwa unataka kuchukua utawala juu ya maisha yako na kuweza kuvifikia vipawa  vingi vilivyopo ndani yako ( wewe una uwezo mkubwa sana uliopo ndani yako) basi nakushauri tu rafiki yangu uchukue hatua mara moja katika kumwendeleza kiongozi aliyepo  ndani yako. Tunahitaji kuwa na viongozi wengi katika jamii zetu. Sasa la kujiuliza hapo ni je, upo tayari kuwa kiongozi ajaye?. Jibu la swali hilo unalo mwenyewe.

Nakutakia kila la kheri katika safari yako ya kuwa kiongozi .Usichoke kutembelea mtandao huu kwa mambo mazuri ya kujifunza na kuhamasika. Pia waalike na wenzako ili nao waweze kupata mambo haya mazuri. Karibu sana rafiki.

No comments

Contact us:Email:godfreymtega@gmail.com/WhatsApp-+255758297744/+255716824009 . Powered by Blogger.