Header Ads

Hatua Nne (4) Za Kuchukua Ili Kuendelea Kufanya Kile Unachokifanya Hata Kama Utakumbwa Na Magumu Kiasi Gani.

Habari za wakati huu ndugu msomaji wa makala za mtandao huu, ni matumaini yangu kuwa unaendelea vizuri. Karibu katika makala ya leo ambayo nataka nikushirikishe juu ya hatua nne za kuchukua ili kuweza kuendelea kufanya kile unachokifanya hata kama utakumbwa na magumu kiasi gani.

Mara nyingi binadamu tumekuwa ni watu wenye kujishughulisha  na mambo mbalimbali, hii yote ni katika kuhakikisha kuwa tunajiletea maendeleo ambayo tumekuwa tukiyataka, lakini wakati ukiendelea kupambana ili kuweza kujiletea mafanikio husika kuna baadhi ya mambo ambayo yanaweza kwenda ndivyo sivyo na hapa ndipo huwa panakuwa na shida kubwa kwani ni watu wachache sana ambao huwa na moyo wa kuendelea na shughuli zao hata kama mambo hayajawaendea vizuri. Kama na wewe ni mmoja wapo wa watu hao basi karibu tujifunze leo hii nini tufanye ili kuweza kubaki  na ile hali ya kufanya shughuli zetu pamoja na magumu tunayopitia.

1. Fikira chanya, siku zote katika maisha yako fikiri mambo chanya, kuwa na fikira kuwa jambo unalolifanya linawezekana japo wengi wanaona kuwa haliwezekani, na namna mojawapo ya kuwa na fikira chanya ni kwa wewe kuacha zile fikira za bendera fuata upepo. Yaani usifanye kitu fulani kwa kuwa wengi wanafanya au usifikiri kwa namna fulani kwa kuwa wengi ndivyo wanavyofikiri hapana badala yake wewe fikiri katika njia nyingine ambayo ni chanya. Ukiwa na fikira chanya basi hii itakusaidia wewe hapo kuweza kubakia katika shughuli husika.

2. Jua unachokitaka, hatua ya pili ya kuweza kukusaidia wewe katika kuweza kubaki katika shughuli yako ni kwako wewe kujua nini unataka. Hapa utahitajika kuelewa kwa undani ni nini unakitaka kutokana na shughuli husika ambayo umekuwa ukiifanya au ambayo unaifanya, jua unachokitaka kutokana na kuajiriwa kwako, jua unachokitaka kutokana na kuwa mkulima, jua unachokitaka kutokana na wewe kuwa mfanyabiashara. Ukishajua unachokitaka basi ama kwa hakika hutohama katika shughuli yako bali utabakia katika shughuli husika siku zote.

3. Tengeneza mpango, shughuli nzuri na yenye kupendeza ni ile ambayo inafanyika chini ya mpango fulani, yaani shughuli iliyo katika mpango fulani yaweza kufanyika kiurahisi sana na kwa kuvutia kuliko shughuli ambayo haijapangiliwa katika mpango wowote ule, ni muhimu kuanzia sasa ukajifunza kupangilia shughuli zako ili tu uweze kuzifanya kwa ubora na zikuvutie wewe mwenyewe. Kuna uwezekano mkubwa sana kuwa kuna baadhi ya watu huondoka katika shughuli zao kwa kuwa tu hawajazipangilia vizuri hivyo haziwavutii hata wao wenyewe na ndio maana huziona kuwa kama shughuli zisizowafaa hata kidogo, kumbe shida haipo katika shughuli bali shida ipo katika mpango wa shughuli husika, hivyo basi kuanzia leo hakikisha unapangilia shughuli yako au zako katika mpango unaoeleweka vyema.

4. Fanya shughuli chache, usiwe mtu wa kufanya shughuli nyingi sana kwa wakati mmoja hii inaweza kuhatarisha utendaji wako wa kazi na hatimae ukakufanya uondoke katika shughuli fulani, hivyo basi hata kama una shughuli kubwa sana hebu anza kwa kufanya shughuli ndogo ndogo ambazo zitakufanya uweze kutimiza ile shughuli kubwa. Kutaka kufanya shughuli kubwa kwa wakati mmoja  wakati mwingine kwaweza kukufanya uone ni kama jambo hilo haliwezekani na matokeo yake ukaamua kuacha kufanya shughuli husika lakini kwa kuchukua hatua za kufanya shughuli ndogo ndogo ili kuweza kutimiza ile shughuli kubwa kutakupa moyo wa kuendelea kutenda.

Nakutakia kila kheri katika kuzifuata hatua hizi.

No comments

Contact us:Email:godfreymtega@gmail.com/WhatsApp-+255758297744/+255716824009 . Powered by Blogger.